advert

http://

Thursday 19 September 2013

MEMBE ASEMA BALOZI WA CHINA ALIFANYA MAKOSA NI HAKI KUCHUKULIWA HATUA NA SEREKALI.



Serikali kupitia Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, imesema kuwa kitendo kilichofanywa na Balozi huyo siyo sahihi na kinakiuka mkataba wa Vienna.


“Wizara inapenda kutamka kwamba kitendo cha Balozi yoyote kuhudhuria mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa na kuvaa sare zenye nembo ya vyama vya siasa siyo sahihi na kinakiuka Kifungu cha 41(1) cha Mkataba wa Vienna wa mwaka 1961, unaoongoza uhusiano wa kidiplomasia,” alisema Membe katika taarifa yake jana jioni.

Taarifa hiyo ilisema kuwa mkataba huo unazuia wawakilishi wa nchi za nje kujihusisha na ushabiki wa kisiasa wanapofanya kazi zao kwenye nchi za uwakilishi. 

“Katika kipindi cha mwaka 2010 hadi 2012, Wizara ilikumbana na vitendo vinavyofanana na kitendo hiki na ikachukua hatua stahiki, kadhalika kwa tukio hili Wizara itachukua hatua za kidiplomasia zinazostahili ili kuzuia jambo hili lisitokee tena,” alisisitiza.

Taarifa hiyo ilisema kuwa Balozi huyo alikwenda wilayani humo kuhudhuria uzinduzi wa mradi wa viwanda vya kuchambulia pamba vinavyojengwa na mwekezaji wa Kichina anayeitwa Tahong, na viwanda hivyo vitakuwa na uwezo wa kuchambua tani 120,000 za pamba kwa mwaka, vitakapokamilika mwakani.

Alisema Wizara imeona picha na habari kwenye vyombo vya habari zikieleza na kumuonyesha Balozi huyo akiwa kwenye mkutano wa CCM.

ALICHOSEMA BALOZI
Balozi huyo amenukuliwa na vyambo vya habari wakati akihutubia mkutano wa hadhara akiwa na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, na kujitahidi kuwasalimia wananchi hao kwa lugha ya kabila la Wasukuma kwa kusema mwadila.

Alisema pamoja na Tanzania kuwa na mfumo wa vyama vingi, anaamini kuwa CCM bado iko imara na inaweza kuendelea kuongoza kwa muda mrefu.

“Kwa hili inadhihirisha kuwa hakuna chama kama CCM kutokana na uimara wake na hili wanalofanya sasa la kuja kuimarisha chama nasi kule China kupitia chama chetu tawala cha CPC (Chama Cha Kikomunisti cha China), tunafanya kama hivi pia. Mwadila, Shinyanga, CCM Oyeeeeee asanteni sana,” alikaririwa akisema.


Source:Nipashe Jumanne

Serikali imesema mabalozi wanaowakilisha nchi zao nchini wanapaswa kutambua kuwa, wanawajibika kuheshimu Mkataba wa Kimataifa wa Vienna unaoainisha taratibu za diplomasia.


Pia, inasema inajiandaa kumwandikia barua Balozi wa China nchini, Lu Younqing kutokana na hatua yake ya kujihusisha na mambo ya siasa.

Wiki iliyopita, Balozi Lu alijitokeza kwenye mkutano wa hadhara wa CCM uliofanyika mkoani Shinyanga, huku akiwa amevalia moja ya sare za chama hicho, hatua ambayo imezusha mjadala miongoni mwa vyama vya siasa na wachunguzi wa mambo ya kidiplomasia.

Akizungumzia kitendo hicho jana, Naibu Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mahadhi Juma Maalim, alisema Serikali inajiandaa kumwandikia barua ya kumkumbusha wajibu wake na kwamba itafanya hivyo baada ya kukusanya taarifa zake.

Hata hivyo, Mahadhi alisema Tanzania na China zitaendelea kuwa marafiki wanaoshirikiana kwenye nyanja mbalimbali kwa shabaha ya kuwaletea maendeleo wananchi wake.

“Hizi taarifa za balozi kuwa kwenye mkutano wa CCM nami zimezisikia na kuziona kwenye vyombo vya habari, tunachokifanya sasa wataalamu wetu wanaendelea kuzifanyia kazi, baadaye tutamwandikia barua kumkumbusha wajibu wake,” alisema.

Alisema siyo vyema kwa mabalozi kushiriki mambo ya kisiasa, kwani kufanya hivyo ni kwenda kinyume na Mkataba wa Vienna ambao ndiyo unaotoa mwongozo.

Pia, Mahadhi aliasa vyama vya siasa kutoachia majukwaa yao yakitumiwa na wanadiplomasia, akieleza kuwa navyo vinawajibika kuheshimu mkataba huo.

Alisema iwapo pande zote zitaheshimu mkataba huo, hakutakuwa na kurushiana lawama.

Mwananchi

Moja ya gari alilokutwa nalo mtuhumiwa.
Jengo ambalo linadaiwa ndiyo kiwanda hatari cha kubadilisha magari ya wizi, kimefumuliwa na mmiliki wake sasa hivi yupo nyuma ya nondo akingoja kufikishwa mahakamani.
Benovilla Luhanga, 43, ametajwa kuwa ndiye mmiliki wa kiwanda hicho na siku ananaswa, alikutwa na magari ya kihafari matano ambayo yote inadaiwa ni ya wizi.
Vilevile, Luhanga alikutwa na Bajaj moja ambayo imedaiwa nayo ni ya wizi na kwamba alikuwa tayari ameshaibadili rangi.

Luhanga alikamatwa akiwa na mkewe ambaye jina lake halikupatikana mara moja.
Kigogo huyo na mkewe, wanaishi ndani ya nyumba hiyo iliyopo Mbezi Beach, Dar es Salaam, kwa nje huonekana kama gereji lakini ndani ni makazi ya watu na shughuli za ubadilishaji magari, Bajaj na pikipiki hufanyika humo.
Luhanga na mkewe walikamatwa baada ya polisi kuvamia kiwanda hicho, saa 5 asubuhi lakini mchakato wa ukamataji ulikamilika saa 10 alasiri.

Mchakato wa kuwakamata uliwagharimu polisi jumla ya saa 5 kukamilika kwa sababu ilibidi kufanya upekuzi wa hali ya juu kwenye kiwanda hicho ili kubeba kila kitu kilichoonekana ni cha wizi.

Magari yote yaliyokutwa kwenye kiwanda hicho pamoja na Bajaj moja, ilidaiwa ni mali za wizi huku tayari yakiwa yameshabadilishwa rangi na kufungwa namba feki za usajili, isipokuwa gari moja.
Gari aina ya Nissan Navara lenye thamani ya shilingi milioni 45 alilokutwa nalo mtuhumiwa.
ZA MWIZI ZILIVYOTIMIA
Habari zinaeleza kuwa kuwa kiwanda hicho kiligundulika kutokana na kijana mmoja ambaye aliwahi kuibiwa gari aina ya Toyota Canter, Goba, Dar, hivi karibuni.

Imebainika kuwa kijana huyo baada ya kuporwa gari hilo ambalo yeye alikuwa ameajiriwa kama dereva, maisha yalimwendea kombo kabla ya kwenda kwa Luhanga kuomba kazi, akidhani ni gereji.

Chanzo chetu kilitamka kuwa akiwa ndani ya kiwanda hicho, kijana huyo aliliona hilo Toyota Canter ndani ya uzio wa kiwanda hicho, hivyo kutoa taarifa Kituo cha Polisi Kawe, Kinondoni, Dar.

“Baada ya kuripoti, askari walifuatilia na kukuta kweli kuna gari aliloibiwa kijana huyo na walipofanya upekuzi wakayakuta magari mengine matano yaliyoripotiwa kuibwa,” kilisema chanzo hicho.

Habari zinasema, polisi waliweza kubaini kuwa magari hayo baadhi yake yalibadilishwa rangi na kupakwa nyeusi huku namba za usajili nazo zikiwa zimebadilishwa.
Nyumba anayoishi kigogo huyo.
KAMATAKAMATA IKAANZA
Polisi baada ya kugundua wizi huo, kamanda aliyeendesha oparesheni hiyo ambaye jina lake halikufahamika mara moja, aliamuru Luhanga na mkewe wakamatwe na magari yaliyokuwa na uwezo wa kutembea yaliendeshwa, mengine yalikokotwa kwa ‘breakdown’ hadi Kituo cha Polisi Kawe.

Uchunguzi umebaini kuwa watuhumiwa hao tayari wamefunguliwa jalada katika kituo hicho kwa namba KW/RB/8194/2013 WIZI WA MAGARI.

Waandishi wetu walipofika kituoni Kawe Jumapili iliyopita, walikuta ndugu sita wa Luhanga wakihaha kutaka kuwawekea dhamana.
MAGARI YALIYOIBWA
Magari yaliyoibwa ni aina ya Nissan Navara lenye thamani ya shilingi milioni 45, lililokutwa na kibao cha usajili namba T519 BNP.

Lingine ni Toyota Harrier, ambalo thamani yake ni shilingi milioni 30. Hili lilikutwa na namba za usajili T 924 AXB, wakati kuna Toyota Rav4 new model, lenye thamani ya shilingi milioni 40 ambalo lilikutwa na namba T 581 BBL.

Gari lingine ni Toyota Canter, vilevile kulikuwa na Rav4 new model nyingine lenye rangi ya kijivu, hili lilikuwa limeng’olewa namba zake halisi bila kuwekewa nyingine.

Rav4 hilo ambayo halikufungwa namba, imeelezwa lilikuwa halijabadilishwa rangi, kwani kwa kawaida yale yanayoporwa na kuingizwa kiwandani humo, hupakwa rangi nyeusi.

OFISINI KWA KAMANDA WA POLISI
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi, Kinondoni, ACP Camillius Wambura, hakuweza kupatikana licha ya waandishi kufika ofisini kwake. Hata hivyo, ofisa mmoja mwandamizi wa jeshi hilo, alithibitisha kutokea kwa tukio.

“Tukio hilo lipo na tunaendelea na uchunguzi,” alisema ofisa huyo huku akiomba asiandikwe jina lake kwa kuwa siyo msemaji wa jeshi hilo.


Stori: Makongoro Oging' na Haruni Sanchawa